Namfua: Singida United imefuzu kwa kuichabanga Yanga goli 4 kwa 2 kombe la shirikisho

PamojaForums · Sep 6, 2026 at 6:36 AMReplies 0 · Views 4
#1
Mechi ya mwisho ya robo fainali imechezwa katika dimba la Namfua, ni mtanange wa kukata na shoka.


DAKIKA 90 ZINAKAMILIKA WANAENDA KIPINDI CHA PENALTI


Dak ya 89, Pigwa hukuu Yanga wanaokoa na kupiga Counter Attack, mpira unakwenda nje


Dak ya 78, Chirwa anashindwa kumalizia vema kazi nzuri ya Tshishimbi, anaupalaza mpira unakwenda nje, goli kiki


Dak ya 75, Piga huku lakini mabeki wa Singida wanaokoa, unarudi kwa Ajib tena unambabatiza na kutoka nje


Dak ya 72, Kevin Yondan anazozana na mchezaji wa Singida, tafurani kidogo inatokea

Dak ya 71, Dante analambwa kadi ya njano, ni kadi ya kujitakia, faulo inapigwa, pigwa huku lakini mpira unaokolewa


Dak ya 57, Mhilu sasa anakwenda na mpira, penyeza kwake Ajib, anapiga krosi huku lakini inaokolewa na Kiggy Makasi

Dak ya 60, Kotinyu anang’aa zaidi eneo la kati hii leo, amekuwa mtulivu kwa dakika zote pale anapopata mpira

Dak ya 55, Singida United 1-1 Yanga


Dak ya 45, Mpira umeanz. Singida wanafanya shambulizi kali dakika hii ya kwanza kipindi cha pili, mpira unakwenda nje


DAKIKA 45 ZA KWANZA ZIMEMALIZIKA, SINGIDA 0-1 YANGA


Dak ya 44, Kutinyu anapewa kadi ya njano, ni ya kwanza katika mchezo huu

Dak ya 43, Kona inapigwa kuelekea Yanga, Kiggy Makasi anapiga lakini inatua kwa kipa Rostand


Dak ya 36, Khalfan na mpira, pasia kwake Kotinyu, gawa pembeni huku Kennedy, inapigwa moja hukuuuu, nje


Dak ya 29, Mvua inazidi kunyesha uwanjani

Dak ya 27, Hatari katika lango la Yanga, pigwa krosi kali na Kutinyu lakini mpira unavuka lango


Dak ya 25, Singida wanarusha baada ya Yanga kuutoa, unarushwa kwake Kontiyu, kwake Nizar Khalfan, piga shuti kali unagongwa kichwa unarudi dimbani


Dak ya 24, Kona inapigwa kuelekea Yanga, namna gani Singida wamekosa nafasi ya kupasia kamba, matokeo ni 0-1


Dak ya 23, Inapigwa… Gooooooooal, Yusuph Mhilu anaiandikia Yanga bao la kwanza kwa njia ya kichwa


Dak ya 21, Mpira unarushwa kuelekea Yanga, kwake Chikupe, piga mbele huku, hataari, kona, inaelekezwa Singida United


Dak ya 20, Gadiel Michael anaondolewa nje ya uwanja baada ya kuumia, mpira unaendelea


Dak ya 19, Kona, Singida wanapata kona ya kwanza, Makasi anakwenda kupiga, piga huku lakini inaokolewa


Dak ya 16, Ajiiib, piga pasi moja ya kunyanyua lakini inakosa mmaliziaji na kutua kwa Barthez kiulaiini


Dak ya 15, Jukwaa la VIP watu wanalowa na mvua inayoendelea kunyesha

Dak ya 14, Kutinyu sasa katikati mwa Uwanja, piga kwake Makasi, Makasi anampasia Mudathir Yahaya, faulo, anachezewa Nizar Khalfan


Dak ya 13, Makapu anapiga mbele kuwatafuta washambuliaji, mpira unakosa mtu, Singida wanauchukua na kuanza upya


Dak ya 12, Andrew Vincent anatolewa nje ya dimba kugangwa baada ya kuumia

Dak ya 10, Ajib anakosa nafasi ya kupachika bao, ilikuwa ni shambulio zuri kwa Yanga, mpira unaendelea

Dak ya 8, Kimvua kinanyesha uwanjani, kila timu inapambana kutafuta goli la mapema

Dak ya 6, Batambuze anaanza kati, piga pasi pembeni huku na mpira unatoka, faulo, inapigwa kwenda Yanga. Imepigwa huku mbelee, kipa Rostand anadaka kama mboga, haikuwa na madhara


Dak ya 5, Faulo imeshapigwa, inagongwa kichwa na wachezaji Singida na kurudi katikati mwa dimba, Tshishimbi anauchukua tena

Dak ya 4, Tshishimbi anachezewa madhambi, inapigwa faulo kuelekea Singida

Dak ya 3, Singida wamepata shambulizi kali la kwanza, lakini linashindwa kuzaa bao, bado 0-0


Dak ya 2, Singida wanaukokota katikati mwa Dimba, Kotinyu anapiga pasi mbele huku lakini Yanga wanaokoa

Dak ya 2, Mpira umeanza punde huku mvua ikiwa inanyesha Uwanja wa Namfua


Dak ya 1, Mpira umeanza


=======


TIMU ya Singida United imefanikiwa kuingia Nusu Fainali ya michuano ya Azam Sports Federation Cup kwa ushindi wa penalti 4-2 baada ya sare ya 1-1 ndani ya dakika 90.


Kiungo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Papy Kabamba Tshishimbi alipiga juu ya lango penalti ya kwanza ya Yanga na winga Emmanuel Martin akagongesha mwamba wa chini kulia mkwaju wake, wakati waliofunga penalti za wana Jangwani hao ni Nahodha Kelvin Yondan na Gardiel Michael.

Kipa wa Yanga, Mcameroon Youthe Rostand alipangua vizuri mkwaju wa Malik Antil lakini akashindwa kuokoa mashuti ya Shafiq Batambuze, Tafadzwa Kutinyu, Kenny Ally na Elinyeswia Sumbi ‘Msingida’.


Katika mchezo huo uliochezeshwa na marefa Hans Mabena kutoka Tanga aliyeasaidiwa na Ferdinand Chacha wa Mwanza na Jesse Erasmo wa Morogoro, hadi mapumziko, Yanga SC walikuwa mbele kwa bao 1-0.

Bao hilo lilifungwa na kinda Yussuf Mhilu, tunda la timu ya vijana ya klabu hiyo, dakika ya 23 kwa kichwa akitumia udhaifu wa beki wa Singida Kennedy Juma Wilson kumalizia kona ya Ibrahim Ajib kutoka upande wa kulia.


Lakini mwanzoni tu mwa kipindi cha pili, dakika ya 46 ya mchezo Singida United wakasawazisha bao hilo kupitia kwa kiungo Kenny Ally Mwambungu aliyepenyezewa pasi nzuri na Mudathir Yahya aliyetumia udhaifu wa wachezaji wa Yanga kuzubaa.


Singida United sasa itakutana na JKT Tanzania iliyorejea Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kuelekea msimu ujao, ambayo jana iliwafunga wenyeji, Tanzania Prisons 2-0 Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.


Nusu Fainali nyingine ya Azam Sports Federation itazikutanisha Mtibwa Sugar iliyoitoa Azam FC kwa penalty 9-8 baada ya sare ya 0-0 na Stand United iliyoichapa Njombe Mji FC 1-0. Juzi mjini Shinyanga.


Kikosi cha Singida United kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Michael Rusheshangoga, Shafiq Batambuze, Juma Kennedy, Malik Antiri, Mudathir Yahya, Nizar Khalfan, Kenny Ally, Lubinda Mundia, Tafadzwa Kutinyu na Kiggy Makassy/Elinyeswia Sumbi dk90+2.


Yanga SC; Youthe Rostand, Juma Abdul/Hassan Kessy dk83, Gardiel Michael, Andrew Vincent, Kelvin Yondan, Said Juma ‘Makapu’/Emmanuel Martin dk65, Yussuf Mhilu, Papy Kabamba Tshishimbi, Obrey Chirwa, Pius Buswita na Ibrahim Ajib.


 
No reactions yetReply / React
Continue the discussion on PamojaForumsOpen full thread